Akizungumza jana Alkhamisi wakati alipokutana na wawakishi wa makabila kutoka mkoa wa Ma'rib, kiongozi wa Ansarullah, Sayyid Abdul Malik Badruddin Al-Houthi amesema vita vya sasa dhidi ya Yemen ni kampeni ya pande zote. Amesema maadui wanatumia mbinu mbali mbali ikiwa ni pamoja na kuzusha mifarakano ili kufikia malengo yao haramu.
Huku akiyapongeza makabila ya mkoa wa Ma'rib kwa kuchukua msimamo ya kitaifa na kusimama kidete katika vita dhidi ya muungano vamizi wa Saudi Arabia na Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), Badruddin Al-Houthi amesema, maadui wameanzisha vita ili kuidhibiti na kuitawala kikamilifu Yemen.
Katibu Mkuu wa Harakati ya Ansarullah ameongeza kuwa, Marekani, utawala haramu wa Israel na Uingereza zimeishinikiza UAE ikithirishwe jinai zake dhidi ya Yemen lakini sasa ni nchi hiyo ya Imarati ndiyo iliyopata hasara na taifa la Yemen linapata ushindi.
Moto wa vita uliowashwa na Saudi Arabia na washirika wake dhidi ya Yemen kuanzia mwezi Machi 2015 na kuendelea hadi sasa umeshapelekea mamia ya maelfu ya watu wasio na hatia kupoteza maisha, mbali na kuwaacha wengine zaidi milioni nne wakiwa hawana pa kuishi.
Uchokozi na uvamzi wa kijeshi wa Saudia dhidi ya Yemen umebomoa na kuharibu zaidi ya asilimia 85 ya miundombinu ya nchi hiyo masikini zaidi katika Bara Arabu na kuisababishia pia uhaba mkubwa wa chakula na dawa nchi hiyo ya Waislamu.