Raisi ameyasema hayo Jumatano asubuhi alipotembelea Haram Takatifu ya Imam Khomeini MA, muasisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa mnasaba wa kuwadia mwaka wa 43 wa ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu. Raisi akiwa hapo pamoja na baraza lake la mawaziri wamesoma Surat al Fatiha na kutoa heshima zao kwa Imam Khomeini MA, muasisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran sambamba na kujadidisha utiifu wao kwa malengo yake matakatifu.
Huku akimtaja Imam Khomeini kuwa 'mwanamabadiliko wa karne', Raisi amesema kuna haja ya kujifunza kuhusu mitazamo ya kisiasa ya Imam ambaye alisisitiza sana kuwahudumia wananchi wa kawaida.
Kwingineko katika hotuba yake,Rais Ebrahim Raisi amesema mashinikizo ya juu kabisa ya Marekani dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran yamefeli kutokana na kampeni ya Iran ya mapambano ya kiwango cha juu kabisa.
Rais wa Iran amesema hata maafisa wa Marekani wenyewe wamekiri kuwa sera zao za mashinikizo ya juu kabisa dhidi ya Iran zimefili. Sera hizo zilianzishwa na rais wa zamani wa Marekani Donald Trump mwaka 2018 na zimeendelezwa wakati wa utawala wa sasa wa Joe Biden.
Raisi amesema wakati maafisa wa Marekani wanapokiri wazi kuwa sera zao mashinikizo ya juu kabisa zimefeli vibaya basi huo ni ushindi kwa taifa la Iran.
Raisi ameendelea kusema kuwa, kila mara wakati Iran inapokabiliana na njama za maadui basi taifa hili hupata ushindi kutoka kwa Mwenyezi Mungu.