Katika mkutano huo uliofanyika Jumapili, IHRC ilijadili ripoti ya hivi karibuni kuhusu Mauaji ya Zaria.
Itakumbukwa kuwa Disemba mwaka 2015, Jeshi la Nigeria liliua kwa umati karibu wafuasi zaidi ya 1000 wa Harakati ya Kiislamu inayoongozwa na Sheikh Ibrahim Zakzaky wakiwemo wanawe watatu na baadaye kuwazika katika makaburi ya umati.
Kadhalika idadi kubwa ya wafuasi wa Sheikh Ibrahim Zakzaky walikamatwa wakati jeshi na vikosi vya ulinzi vya a vilipofanya jinai na ukandamizaji mkubwa dhidi ya ofisi za Harakati ya Kiislamu ya Nigeria (IMN)
Uvamizi huo ulijiri baada ya Jeshi la Nigeria kudai kuwa wafuasi wa Harakati ya Kiislamu walikuwa na njama ya kutaka kumuua mkuu wa jeshi hilo, madai ambayo yalikanushwa vikali na wafuasi wa harakati hiyo.
Ripoti ya hivi karibuni ya IHRC kuhusu Mauaji ya Zaria inaonyesha kuwa serikali ya Nigeria iko mbioni kufuta kabisa ushahidi wa matukio ya Disemba 2015 na hivyo imetoa wito kwa Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC) ichukue hatua kabla ya ushahidi wote kufutwa.
Kikao hicho cha video kimewashirikisha mwandishi wa ripoti hiyo ya IHRC Caterina Aiena, mkuu wa timu ya mawakili wa Sheikh Zakzaky, Femi Falana, mtu aliyeshuhudia mauaji ya Zaria, Jummai Karofi, daktari aliyeongoza timu ya madaktari waliomtembelea Sheikh Zakzaky mwaka jana, Daktari Kazim Dallah na bintiye Sheikh Zakzaky, Suhaila. Kikao hicho kiliendeshwa na Raza Kazim.
Sheikh Ibrahim Zakzaky, (66) na mkewe Malama Zeenat walitiwa nguvuni tarehe 13 Desemba 2015 wakati wanajeshi wa Nigeria walipovamia Hussainia ya Baqiyatullah na nyumba ya mwanazuoni huyo katika mji wa Zaria.
Wanaharakati na wapigania haki katika maeneo mbalimbali ya dunia wanaendelea kuitaka serikali ya Rais Muhamadu Buhari imuachilie huru Sheikh Ibrahim Zakzaky na mkewe.