Akizungumza katika mkutano mjini Tehran na ujumbe wa wanazuoni na wanafikra kutoka vyuo vikuu vya Uturuki, Hujjatul Islam Hamid Shahriari alisema kuanzishwa kwa Umoja wa nchi za Kiislamu kama ulivyo Umoja wa Ulaya (EU) kunaweza kuonekana kuwa ni ndoto lakini linaweza kufikiwa.
Kunaweza kuwa na muungano sio tu katika nyanja za kiuchumi na kitamaduni lakini pia katika masuala ya kisiasa na kidini, alisema, na kuongeza muungano huo hauna maana ya kutupilia mbali katiba au kuondoa mipaka ya nchi.
“Tunaweza kuelekea kwenye mwelekeo huo kwa hekima,” akasema.
Mwanazuoni huyo wa Kiislamu alisisitiza umuhimu wa umoja katika ulimwengu wa Kiislamu na kusema ikiwa kuna umoja kati ya nchi kama Iran, Saudi Arabia na Uturuki, basi itawezekana kuwa na muungano wa Kiislamu wenye nguvu duniani.
Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Kimataifa ya Kukurubisha Madhehebu za Kiislamu, yenye makao yake Tehran, pia alitoa wito wa kuundwa kwa bunge la pamoja la nchi za Kiislamu ili kupitisha sheria za pamoja.
Aidha amesema ili kuzuia mifarakano na misuguano, kuna ulazima wa kuzuia vita na ukufurishaji katika ulimwengu wa Kiislamu.
Ameendelea kusema kuwa iwapo Waislamu watakuwa na urafiki na watatendeana mema basi watafanikiwa katika kukabiliana na adui wao wa pamoja.