IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Ghasia nchini Iran ziliratibiwa na Marekani pamoja na utawala wa Kizayuni

22:54 - October 03, 2022
Habari ID: 3475872
TEHRAN (IQNA)- Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza katika hafla ya pamoja ya wanachuo wahitimu wa Vyuo Vikuu vya vikosi vya ulinzi nchini Iran kwamba ghasia na machafuko yaliyoshuhudiwa hivi karibuni hapa nchini yaliratibiwa na Marekani na utawala ghasibu na bandia wa Kizayuni na kusaidiwa kwa hali na mali na mabwana zao na baadhi ya wasaliti raia wa Iran wanaoishi nje ya nchi.

Kwa mujibu wa Kitengo cha habari cha Ofisi ya  Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, Ayatullah Khamenei ameashiria leo katika hotuba muhimu aliyoitoa kwenye hafla ya pamoja ya wanachuo wahitimu wa Vyuo Vikuu vya vikosi vya ulinzi kuhusu matukio ya karibuni hapa nchini na kusisitiza kuwa: Wananchi wa Iran wamejitokeza kwa nguvu zote kikamilifu katika matukio hayo pia kama ilivyokuwa katika matukio mengine ya huko nyuma; na katika siku za usoni pia watafanya kama walivyofanya hivi karibuni.  Amesema katika siku za usoni pia, wananchi shujaa na wachaMungu wa Iran watailinda nchi kwa nguvu zote popote pale maadui watakapodhamiria kuibua machafuko na ukosefu wa amani hapa nchini. 

Kiongozi Muadhamu amesema taifa la Iran kama alivyo kiongozi wao Amirul Muminin,  Ali (AS) ni taifa madhlumu na wakati huo huo ni taifa lenye nguvu na kuongeza kuwa: Katika tukio hilo lililojiri hivi karibuni, binti kijana ameaga dunia ambapo mioyo yetu pia imehuzunika na kukumbwa na majonzi lakini hazikuwa hatua na radiamali za kawaida pale baadhi ya watu walipoamua kuchukua hatua mkabala wa tukio hilo bila kufanya uchunguzi yaani kundi la watu lilipoingia mitaani na kuibua fujo na ghasia, kuchoma moto Qurani Tukufu, kumvua mwanamke vazi lake la hijabu na kuteketeza msikiti, husseiniya na magari ya watu. 

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu aidha amesisitiza kuwa, ghasia hizo zilikuwa zimeratibiwa kitambo nyuma; kwani wachochea machafuko walipanga kuibua ghasia na ukosefu wa amani hapa nchini tarehe Mosi mwezi Mehr (23 Septembe) mwaka huu kupitia kuibua kisingizio kingine hata kama lisingekuwepo suala la binti huyo kijana.

Ayatullah Khamenei amebainisha kuwa ghasia na machafuko mengi hutokea katika maeneo mbalimbali duniani; na huko Ulaya na hasa huko Paris nchini Ufaransa ghasia zimekuwa zikishuhudiwa mara kwa mara. Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu aidha amesisitiza kuwa, matamshi yaliyotolewa na viongozi wa Marekani kwamba wamesikitishwa na kuaga dunia binti huyo tajwa ni  ya uwongo.

Amesema hapa nchini wakuu wa mihimili mitatu ya dola wameeleza kusikitishwa na tukio hilo ambapo Idara ya Mahakama ya Iran imeahidi kuwa itafuatilia kadhia hiyo hadi mwisho.

Katika upande mwingine, Ayatullah Khamenei ameashiria kupiga hatua maendeleo ya nchi katika sekta zote na kufanyika juhudi za kuhuisha uzalishaji na uwezo wa ndani ya nchi kwa ajili ya kusambaratisha vikwazo na kusisitiza kuwa: "Maadui hawataki kuona hatua za maendeleo zikipigwa hapa nchini; na ndio maana wameratibu mipango ya kufunga Vyuo Vikuu, kuibua ghasia na fujo na kuwatumbukiza viongozi katika kadhia mpya huko kaskazini magharibi na kusini mashariki mwa nchi ili kusitisha harakati zote hizi."    

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza kuwa, Marekani si tu inaipinga Jamhuri ya Kiislamu ya Iran bali inapinga Iran iliyo imara na iliyo huru. Ameongeza kuwa, viongozi wa Marekani wanaitaka Iran ile iliyokuwepo wakati wa zama za utawala wa kifalme wa Pahlavi; ambayo ilikuwa ikitii amri na matakwa yao kama ng'ombe anayekamwa maziwa. 

4089411

captcha