IQNA

Mwanazuoni wa Kiislamu Uingereza atoa fatwa kuhusu kuchangia viungo vya mwili

17:07 - June 22, 2019
Habari ID: 3472011
TEHRAN (IQNA) – Mwanazuoni wa Kiislamu nchini Uingereza amechapisha fatwa mpya kuhusu kuchangia viungo vya mwili.

Fatwa hiyo inatazamiwa kuweka wazi mtazamo wa Uislamu kuhusu iwapo Muislamu anaweza kuamuru viungo vyake vipewe wagonjwa ambao wanahitaji baada ya yeye kuaga dunia.
Mufti Mohammad Zubair Bhutt, ambaye ni mwanazuoni wa ngazi za juu wa Kisunni amechunguza taratibu zilizopo hivi sasa za kuchangia viungo vya mwili katika jamii ya Waislamu, na baada ya kushauriana na wanazuoni wenzake Uingereza, Maimamu na taasisi za Waislamu, ametangaza fatwa ya mtazamo wa Kisunni ili kuwaongoza Waislamu katika kadhia ya kuchangia viungo.
Hii si fatwa ya kwanza kuchapishwa Uingereza kuhusu kuchangia viungo vya mwili, kwani mwaka 1995 na 2000 kulitolewa fatwa kuhusu kadhia hii.
Fatwa mpya iliyotangazwa imetegemea fiqhi ya Kiislamu ya madhehebu nne mashuri za Kisunni za Hanafi, Maliki, Shafii na Hanbali.
Sehemu ya fatwa hiyo kuhusu viungo vya mwili wa binadamu inasema : "Viungo bandia vinajuzu. Inajuzu kupandikiza viungo vya wanyama wasio najisi na pia inajuzu kupandikiza tishu za wanayma wasio najisi lakini haijuzu kupandikiza viungo na tishu za wanyamya najisi isipokuwa tu pale hakuna mbadala unaojuzu. Inajuzu kupandikiza viungo na tishu za binadamu. Mtu aliyehai anaruhusiwa kuchangia kiungo chake cha mwili maadamu madhara atakayoyapata ni madogo mno na maadamu hatapoteza maisha."
Fatwa hiyo imetolewa baada ya miaka mingi ya utafiti na kwa uungaji mkono wa Huduma ya Kitaifa ya Afya ya Uingereza, maarufu, National Health Service (NHS).
Mufti Zubair Bhatt amesema anatumai kuwa fatwa hiyo itaweka wazi masuala mengi kuhusu uhalali wa kuchangia viungo vya mwili na itawawezesha Maimamu na wahubiri Waislamu kujadili suala hilo na jamii za Waislamu.
Kuna zaidi ya Waislamu zaidi ya milioni 2.7 nchini Uingereza, na kwa muda mrefu wale wanaohitaji figo au maini wamekuwa wakilizamika kusubiri kwa muda mrefu zaidi kuliko wale ambao si Waislamu.
Fatwa hii mpya inatazamiwa kuwashawishi Waislamu zaidi wajaribu kuchangia viungo hivi muhimu wakiwa hai ama waruhusu viungo vya wapendwa wao wanaofariki kutumika.

3468791

captcha